
Mabingwa: Bayern Munich wakisherehekea taji lao la Ligi ya Mabingwa baada ya kuifunga Borussia Dortmund



WINGA Arjen Robben ameuzika mzimu wa
kukosa penalti msimu uliopita katika fainali ya Ligi ya Mabingwa dhidi
ya Chelsea, baada ya usiku huu kuifungia bao la ushindi Bayern Munich
katika fainali ya michuano hiyo Uwanja wa Wembley, London, England
ikishinda 2-1 na kutwaa Kombe hilo.
Bayern sasa wanakuwa mabingwa wapya wa
Ulaya, wakirithi taji lililoachwa wazi na Chelsea kwa ushindi wa 2-1
dhidi ya Wajerumani wenzao, Borussia Dortmund katika mchezo mkali na wa
kusisimua.
Mholanzi huyo alifunga bao hilo tamu
dakika ya 89, baada ya awali kipindi cha kwanza kukosa mabao mawili ya
wazi. Lakini ndiye aliyetoa pasi ya bao la kwanza kwa Bayern
lililofungwa na Mario Mandzukic dakika ya 60.
Dortmund ilisawazisha kwa penalti baada
ya Dante kumuangusha kwenye eneo la hatari Marco Reus na Ilkay Gundogan
akaenda kufunga dakika ya 67.
Katika mchezo huo, uliochezeshwa na refa Nicola Rizzoli kutoka Italia, kikosi cha Bayern kilikuwa; Neuer,
Lahm, Boateng, Dante, Alaba, Javi Martinez, Schweinsteiger, Robben,
Muller, Ribery/Gustavo dk90+1 na Mandzukic/Gomez dk90+4.
Borussia Dortmund: Weidenfeller,
Piszczek, Subotic, Hummels, Schmelzer, Bender/Sahin dk90+1, Gundogan,
Blaszczykowski/Schieber dk90+1, Reus, Grosskreutz na Lewandowski.

Bao la ubingwa: Arjen Robben amekuwa shujaa wa fainali ya Ligi ya Mabingwa usiku huu








No comments:
Post a Comment